UTANGULIZI
Dunia imepitia mapinduzi ya aina mbalimbali ambayo yamekuwa yakitumika kutambulisha zama. Tumepitia mapinduzi kama yale ya kilimo na ya viwanda. Hivi sasa tuko, jamii zingine ziko njiani kuingia, katika zama za habari na mawasiliano. Zama hizi zinatokana na mapinduzi katika zana za habari na mawasiliano. Mapinduzi haya yanawezesha watu wa kawaida kufanya mambo ambayo huko nyuma yalikuwa yakifanywa na makampuni makubwa au watu wenye fedha..
Kwa mfano, ungetaka kuwa na gazeti au redio ilikuhitaji kuwa na mtaji mkubwa wa kununua vifaa, kukodi au kununua jengo la ofisi, fedha za kulipa wafanyakazi, kama ni gazeti uwe na fedha za kulichapisha na mtandao wa kulisambaza, kama ni gazeti unahitaji fedha za kununulia mitambo, halafu kuna usajili chombo chako (ambapo kwenye nchi zetu zoezi la kusajili limetawaliwa na ukiritimba na rushwa).
Katika zama hizo, wananchi tunaambiwa kuwa tuna uhuru wa kutoa mawazo na kujieleza lakini hakukuwa na zana au nyenzo za kutuwezesha kusambaza mawazo yetu au kupokea mawazo ya wananchi wengine kama sisi. Watu wengine wanaweza kupata nafasi hapa na pale kutoa mawazo yao kama kupitia safu ya barua za wasomaji. Lakini tunajua kuwa barua nyingi hazisomwi. Zinatupwa. Na wakati mwingine barua za wasomaji sio za wasomaji bali ni za waandishi wenyewe! Wakati mwingine tunapata nafasi ya kupiga simu redioni lakini ukweli ni kuwa hatuna mamlaka ya kuamua vipindi viendeshwe vipi. Unachopata ni nusu dakika ya kusikika redioni.
Sasa tuko katika zama ambazo zipo nyenzo/zana zinazokuwezesha wewe na mimi kuwasiliana na umma bila kupitia chombo cha mtu mwingine (kama simu redioni, barua za wasomaji, au safu gazetini). Unaweza kuwa na chombo chako mwenyewe. Kwahiyo ukitumia blogu ya maandishi, ni sawa na kuwa na gazeti lako. Ukitumia blogu ya sauti ni sawa na kuwa na redio yako. Kwa kutumia blogu ya picha za video ni sawa na kuwa na kituo chako cha luninga. Haya ni mapinduzi makubwa sana, mapinduzi ya zana hizi kuwa mikononi mwa umma. Haya ni mapinduzi kwani unachohitaji ili ufanye niliyosema hapo juu (yaani kuwa na chombo chako mwenyewe cha habari) ni dakika tano. Na mwongozo huu kazi yake ni kukusaidia kufanya hivyo.
Kwahiyo huu ni mwongozo kwa mtu yeyote yule ambaye ana jambo la kusema au ana nia ya kutumia haki yake ya msingi ya kujieleza kwa kutumia teknolojia mpya na rahisi ya blogu. Huu ni mwongozo wa wale wasio na blogu na pia wale ambao tayari wana blogu. Upo mjadala unaondelea kutafuta jina muafaka la teknolojia hii. Bonyeza hapa ufuatilie mjadala huo. Kwakuwa bado hatujalipata, nitatumia neno blogu katika mwongozo huu.
Kama una swali lolote ambalo hujapata jibu lake hapa, usisite kuniuliza mimi kupitia anuani hii: ughaibuni@yahoo.com. Unaweza pia kuwasiliana na mwanablogu yeyote wa Kiswahili. Wanablogu wote wana nia ya kuhamasisha watu zaidi kutumia teknolojia hii hivyo usijisikie kuwa utakuwa unawasumbua.
Mtu yeyote anaweza na ana haki ya kuwa na blogu, awe mwandishi, mcheza mpira, mwalimu, mwanamuziki, dakitari, mwanasiasa, mkulima, misheni tauni, n.k. Blogu ni njia rahisi sana ya kutoa habari, maoni, kujenga mtandao, kupeana maarifa, elimu, n.k. Unachotakiwa kufanya ni kutazama upande wa kuume ambapo kuna orodha ya yaliyomo. Hapo utachagua kipengele cha mwongozo unachohitaji.
May 5, 2007 at 9:41 am |
a free project for a tanzanian young peole \,to practise awareness and promoting actual behaviour change
June 14, 2007 at 12:15 pm |
To meet the people and try to exchange views.
October 30, 2007 at 12:54 pm |
to establish a maabara ya migodi ya dhahabu kwa tanzania
November 5, 2007 at 12:43 pm |
It is realy that respecting all people is a one way to keep up ur own future in good manner.